Sunday, December 04, 2016

CHUO KIKUU ARDHI CHAKAMILISHA UJENZI NA UWEKAJI VIFAA BANDARI YA TANGA

 Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, Prof. Idrissa Mshoro akiwasili katika viwanja vya chuo hicho kwa ajili ya kuhudhuria katika mahafali ya 10 ya chuo hicho yaliyofanyika jana Jijini Dar es Salaam.
tanga-1
Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, Mhe. Cleopa Msuya akimtunuku mmoja wa wanafunzi wa shahada ya Udaktari wa Falsafa (PhD) aliyoipata katika chuo hicho. Mahafali hayo yamefanyika jana Jijini Dar es Salaam katika viwanja vya chuo hicho.
tanga-2
Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, Mhe. Cleopa Msuya (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wengine waliohudhuria kwenye mahafali ya 10 ya chuo hicho akiwemo Kaimu Mwenyekiti wa Baraza la chuo hicho, Prof, Evelyne Mbede (wa pili kushoto), wa tatu kulia ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhandisi Stella Manyanya. Mahafali hayo yamefanyika jana Jijini Dar es Salaam katika viwanja vya chuo hicho.
tanga-3Baadhi ya wanafunzi wa shahada na stashahada waliohitimu katika chuo hicho wakiwa katika viwanja vya chuo. Mahafali hayo yamefanyika jana jijini Dar es Salaam.
…………………..
           Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Chuo Kikuu Ardhi kimekamilisha ujenzi na uwekaji wa vifaa katika Bandari ya Tanga ikiwa ni moja ya miradi ya kiutafiti inayofanywa chuoni hapo kwa ajili ya kupima hali halisi ya bahari.
Makamu wa Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Idrissa Mshoro ameyasema hayo alipokuwa akisoma hotuba wakati wa mahafali ya 10 ya chuo hicho yaliyofanyika jana chuoni hapo jijini Dar es Salaam.
Prof. Mshoro amesema kuwa pamoja na jukumu la kutoa wahitimu katika fani mbalimbali kwa maendeleo ya nchi pia chuo hicho kina majukumu ya kufanya utafiti na kutoa ushauri wa kitaalam hivyo kupitia Mradi wa Utafiti wa Mabadiliko ya Tabia Nchi uliofadhiliwa na Serikali ya Norway kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania umeweza kufanikisha ujenzi huo.
“Madhumuni ya Mradi huu ni kusaidia kuboresha mawasiliano kati ya Bandari na watumiaji wake kwani taarifa sahihi zitakazotolewa kuhusu hali halisi ya bahari zitasaidia kufanya maamuzi sahihi ya kutumia Bandari hiyo pia, taarifa hizo zitakuwa msaada mkubwa kwa wadau wengine kama wavuvi, watalii pamoja na watafiti mbalimbali,” alisema Prof. Mshoro.
Ameongeza kuwa katika kutoa ushauri na huduma za kitaalam, chuo kimetekeleza miradi mbalimbali ya Serikali, taasisi za Umma na Binafsi katika fani zote zinazofundishwa chuoni hapo hivyo kusaidia katika kuongeza kipato cha chuo kwa ajili ya miradi, kutoa motisha kwa wafanyakazi pamoja na kutoa fursa kwa wana taaluma kupata uzoefu kwa vitendo katika fani mbalimbali walizosomea.
Aidha, Prof. Mshoro ameishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuendelea kukipatia chuo fedha na misaada mingine kwa ajili ya kuendeshea shughuli za chuo ambapo kwa mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali imetengea jumla ya shilingi bilioni 5 kwa ajili ya bajeti ya maendeleo ya chuo hicho.
Akiongelea kuhusu wahitimu, Prof.  Mshoro amefafanua kuwa jumla ya wanafunzi 968 watatunukiwa shahada na stashahada mbalimbali ambapo wanafunzi 868 watatunukiwa shahada za awali, 80 shahada za uzamili, 14 watatunukiwa stashahada pamoja na shahada za uzamivu kwa wanafunzi 6.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhandisi Stella Manyanya amesema kuwa bado kuna changamoto kubwa kwa wasichana kujiunga na masomo ya sayansi kwani idadi imeonyesha kuwa wahitimu wa kike ni 320 ambayo ni sawa na asilimia 33 ya wanafunzi wote hivyo ametoa rai kwa wasichana kutumia fursa za kusomea masomo hayo bila kuogopa.
Mhandisi Manyanya amewashauri vijana kujikita kusoma masomo yatakayowapelekea kujiajiri wenyewe kuliko yale yanayohitaji kuajiriwa kwani njia hiyo itasaidia kujikwamua kiuchumi kwa haraka na kuchangia katika maendeleo ya taifa.

No comments: