Thursday, October 13, 2016

Wachimbaji wa Madini watakiwa kujipatia Elimu na Teknolojia sahihi

Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Prof.Justin Ntalikwa na Katibu Mtendaji Baraza la Taifa uwezeshaji wananchi kiuchumi Bi.Beng’i Issa wakipata maelezo toka kwa Bi Shamsa Diwani wa kikundi cha MIVA kinachojiusisha na uchimbaji mdogo wa madini na usio rasmi leo jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano kazi wa wadau wanawake katika sekta ya madini.
Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Prof.Justin Ntalikwa na Katibu Mtendaji Baraza la Taifa uwezeshaji wananchi kiuchumi Bi.Beng’i Issa wakipata maelezo toka kwa Bi Susan Fred wa TAMICUSO ambao wanajiusisha na uchimbaji mdogo wa madini ya Tanzanite jijini Arusha.
Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Prof.Justin Ntalikwa akiuliza swali kwa Bi Martha Kayaga wa kikundi cha WAWACHISI tokea singida jinsi wanavyochimba madini ya gypsum na kuyahifadhi katika mkutano wa wadau wanawake katika sekta ya madini.Kulia ni Katibu Mtendaji Baraza la Taifa uwezeshaji wananchi kiuchumi Bi.Beng’i Issa.
Katibu Mtendaji Baraza la Taifa uwezeshaji wananchi kiuchumi Bi.Beng’i Issa akizungumza na wanawake wachimbaji madini wadogo wadogo(hawapo pichani) leo katika ukumbi wa Mwalimu Nyerere walipokutana katika mkutano kazi wa wadau wanawake katika sekta ya madini.
Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Prof.Justin Ntalikwa akizungumza jambo na Katibu Mtendaji Baraza la Taifa uwezeshaji wananchi kiuchumi Bi.Beng’i Issa,Bi Tertula Swai wa UN women na Kessy Edward wa Baraza la Taifa uwezeshaji wananchi kiuchumi.

Picha na Daudi Manongi,MAELEZO


Na Daudi Manongi,MAELEZO.

Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Profesa Justin Ntalikwa ametoa wito kwa wachimba wadogo wadogo wa madini kuongezea juhudi katika uchimbaji wa madini ikiwa ni pamoja na kujipatia elimu ya uchimbaji sahihi wa madini na kutumia teknolojia nzuri ambayo itawasaidia kuongeza tija katika shughuli zao.

Profesa Ntalikwa ameyasema hayo wakati akifungua mkutano kazi wa wadau wanawake katika sekta ya madini wanaojihusisha na uchimbaji ambao sio rasmi na mdogo uliofanyika katika viwanja vya Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.

“Mimi wito wangu kwa wachimbaji hawa ni kwamba nawaomba wajipatie elimu na teknolojia sahihi ili waweze kujiongezea kipato katika uchimbaji huu”,Alisema Prof Ntalikwa.

Aidha Katibu Mkuu uyo aliwataka wachimbaji wadogo wadogo hao kuwasiliana na Baraza la Taifa la uwezeshaji wananchi kiuchumi(NEEC) kwa ajili ya kuwasaidia sehemu ambazo ambazo wanaweza kupata mitaji maana suala la mtaji ni muhimu sana ili waweze kuboresha shughuli za uchimbaji.

Pia amesema kuwa serikali imeanza kutoa ruzuku kwa awamu kwa wachimbaji hawa wadogo wa madini na hivi sasa wanajipanga kutoa awamu ya tatu ya ruzuku ikiwa na lengo ya kuwasaidia kununua vifaa vya uchimbaji na teknolojia sahihi itakayorahisisha uchimbaji wa madini na kuongeza kuwa kwa sasa wameshapokea maombi kutoka kwa wachimbaji mbalimbali na wanayafanyia kazi ili wapate washindi watakaojipatia ruzuku.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji Baraza la Taifa uwezeshaji wananchi kiuchumi Bi.Beng’i Issa amesema kuwa wao kama baraza watatengeneza programu ya jinsi ya kupata uongozi kwa wachimbaji hao ambao utasaidia kuwakilisha mawazo yao serikali na pia program ya kuwajengea uwezo pale ambapo wachimbaji hawa wana mapungufu na pia kuwaunganisha na masoko kama vile viwanda vya ndani ili visinunue malighafi kutoka nje na badala yake wanunue hapa nchini malighafi yanatotokana na uchimbaji wa madini.

No comments: