Friday, October 07, 2016

Tanesco yatakiwa kutumia nguzo za zege


Na Greyson Mwase, Mtwara 

Ili kuondokana na adha ya kuharibiwa kwa miundombinu ya umeme ikiwa ni pamoja na nguzo kuchomwa na moto pindi wananchi wanaposafisha mashamba, Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) limetakiwa kuanza matumizi ya nguzo za zege badala ya nguzo za miti. 

Hayo yalielezwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Profesa Justin Ntalikwa alipokuwa akizungumza na uongozi wa TANESCO mkoa wa Mtwara alipokuwa katika ziara ya siku tatu katika mkoa huo kwa ajili ya kukagua shughuli za nishati husuan maeneo gesi inapozalishwa pamoja na madini. 

Alisema kumekuwepo na changamoto ya nguzo za umeme kuchomwa moto hususan katika kipindi cha kiangazi wananchi wanaposafisha mashamba yao, sehemu nyingi nchini husuan katika maeneo ya vijijini. 

Alisisitiza kuwa pamoja na elimu kutolewa kwa wananchi juu ya utunzaji wa miundombinu ya umeme hususan nguzo, bado kuna haja ya TANESCO kuwa wabunifu kwa kuanza kutumia nguzo za zege ambazo haziungui kwa haraka na kuepusha hasara ya kuchomwa na moto 

“ Fedha inayotumika kwa ajili ya kurudisha nguzo zilizochomwa na moto ingeweza kupeleka umeme katika maeneo mengine ambayo hayana huduma ya umeme,”alisema Profesa Ntalikwa. 

Aidha, aliwataka watumishi wanaofanya kazi katika ofisi za TANESCO kuacha mazoea ya kukaa ofisini na kusubiri wateja na badala yake wanatakiwa kuwafuata wateja majumbani na kuwashawishi kuunganishwa na huduma za umeme. 

“ Ni lazima mhakikishe shirika la TANESCO linaongeza mapato yake na kujiendesha kwa faida na sio kwa hasara, muwafuate wateja majumbani badala ya kukaa ofisini tu,” alisisitiza Profesa Ntalikwa. 

Pia, Profesa Ntalikwa aliwataka watumishi wa TANESCO kuhakikisha kuwa wateja wanaoomba na kulipia huduma za kuunganishiwa umeme wanaunganishiwa ndani ya mwezi mmoja badala ya kukaa kwa muda mrefu hali inayokatisha tamaa. 

Alisema kuwa mteja ana haki ya kuunganishiwa huduma ya umeme kwa wakati pindi anapokamilisha taratibu zote za malipo. 

Awali akizungumzia hali ya umeme na utekelezaji wa miradi ya umeme katika mkoa wa Mtwara kupitia taarifa yake, Meneja wa Shirika la Umeme Mkoa wa Mtwara, Mhandisi Azizi Salum alisema kuwa umeme unaotumika katika mikoa ya Lindi na Mtwara unazalishwa kutoka katika mitambo ya TANESCO iliyopo Mtwara Mjini inayotumia gesi ambapo kwa sasa inazalisha Megawati 18 huku matumizi ya juu yakiwa ni Megawati 15.1 

Alisema kuwa, hadi kufikia mwezi Septemba, mwaka huu mkoa ulikuwa na jumla ya wateja 30,457 ambapo wateja wakubwa katika mkoa wa Mtwara wakiwa ni 44. 

Akielezea jitihada zilizofanywa na shirika la TANESCO katika upunguzaji wa matukio ya kukatika kwa umeme katika wilaya za Lindi na Mtwara, Mhandisi Salum alieleza kuwa ni pamoja na ubadilishaji wa nguzo chakavu na vikombe vilivyopasuka katika maeneo ya Newala kuelekea Masasi hadi Ndanda ambapo kati ya Julai na Septemba mwaka huu jumla ya nguzo 300 zilibadilishwa. 

Aliendelea kusema kuwa kazi nyingine zilizofanywa ni pamoja na ufungaji wa vikata umeme kwenye vipande vya njia za umeme vilivyo virefu na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovolti 132 yenye urefu wa kilometa 80 na ufungaji wa transfoma ya ukubwa wa 20MVA 132/33kV eneo la Migoyo ili kuboresha upatikanaji wa umeme katika manispaa ya Lindi na wilaya za Masasi, Nachingwea na Ruangwa. 

Aidha, akielezea miradi mingine ya umeme iliyotekelezwa katika mkoa wa Mtwara, Mhandisi Salum alitaja miradi hiyo kuwa ni pamoja ujenzi wa miundombinu ya umeme vijijini chini ya ufadhili wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ambao ulihusisha ujenzi wa njia ya umeme Msongo wa kilovolti 33 wenye jumla ya kilometa 213 na ufungaji wa transfoma 38 ambapo gharama ya mradi ilikuwa ni shilingi bilioni 9.477 na kuongeza kuwa ulikamilika mwezi Juni mwaka huu 

Miradi mingine ni pamoja na mradi wa kupeleka umeme kwenye wilaya za Tandahimba, Mtwara Vijijini na maeneo yaliyo katika mkuza wa bomba la gesi chini ya mkandarasi Namis Corporate LTD 

Alisema mradi huu wenye gharama ya shilingi bilioni 19 unahusisha ujenzi wa kilometa 304.92 za msongo wa kilovolti 33, ufungaji wa transfoma 106, ujenzi wa njia za kusambazia umeme jumla ya kilometa 265.15 na kuunganisha wateja 9,037 katika vijiji na vitongoji 83 

Alisisitiza kuwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2016/17 shirika la TANESCO limetenga kiasi cha shilingi bilioni 1.078 kwa ajili ya kusambaza huduma ya umeme katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Mtwara.

No comments: