Wednesday, August 31, 2011

Rais Kikwete katika sherehe za Idd Dar, baraza la Iddi Dodoma

Sheikh Mkuu na mufti wa Tanzania Issa bin Shabaan Simba akimkaribisha katika baraza la Iddi Rais Jakaya Mrisho Kikwete lililofanyika katika msikiti wa Gaddafi Mkoani Dodoma (picha na Freddy Maro).

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwapa mkono wa Iddi baadhi ya waumini waliohudhuria swala ya Iddi katika msikiti wa Kichangani uliopo Magomeni Mapipa jijini Dar es Salaam leo asubuhi(picha na Freddy Maro)


Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwasalimu waumini waliohudhuria swala ya Iddi katika msikiti wa Kichangani uliopo Magomeni Mapipa jijini Dar es Salaam leo asubuhi.

Sunday, August 28, 2011

Futari kwa Makamu wa Rais Dk Bilal

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Mohammed Gharib Bilal, akiagana na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Issa Shaaban Simba, baada ya kumalizika kwa hafla ya futari iliyoandaliwa na Makamu katika makazi yake Oysterbay Dar es Salaam

Rais Dk Jakaya Kikwete, Makamu wake Dk Mohammed Gharib Bilal, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadick, wakiomba dua kwa pamoja baada ya kupata futari iliyoandaliwa na mwenyeji wao. Picha ya VPO.

Maelfu ya watu wakwama Kilombero, Ulanga

MV Kilombero (ii), MV Kilombero - II, MV kilombero II, MV Kilombero

Baadhi ya abiria wakitoka katika kivuko cha MV Kilombero II upande wa wilaya ya Kilombero wakitokea upande wa wilaya ya Ulanga. (Picha zote na Venance George)
MAELFU ya watu na zaidi ya magari 300 yamekwama kwenye kivuko cha mto Kilombero, mkoani Morogoro, kwa siku tatu sasa kufuatia vivuko viwili vinavyotoa huduma mtoni hapo cha Mv Kilombero I na Mv Kilombero II kupata hitilafu.
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Evarist Ndikilo, alisema vivuko hivyo vimepata hitilafu kufuatia kina cha maji kupungua na kusababisha kukita chini kwenye gati ya upande wa Wilaya ya Ulanga.
Ingawa jitihada za kufukua mchanga hufanywa mara kwa mara kuviwezesha vivuko hivyo kuengeshwa, lakini hatua hiyo imetafsiriwa kuchangia vivuko hivyo kugonga kwenye gati na kusababisha hitilafu.
Ndikilo alisema kivuko cha Mv Kilombero II kilipata hitilafu ya kupasuka moja ya injini zake Agosti 26, hivyo kulazimika kusitisha safari.
Alisema kwa vile mto huo kuna vivuko viwili, Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Omar Chambo, aliagiza kivuko cha zamani cha Mv Kilombero I kuanza kufanya kazi mara moja, huku Wakala wa Ufundi na Umeme (Tamesa) akiagizwa kuanza kukifanyia matengenezo kivuko kilichoharibika.
Hata hivyo, Ndikilo alisema kivuko cha zamani nacho jana kilipata hitilafu ya kutoboka moja ya matangi ya hewa na kuanza kuingiza maji, hali aliyodai ingeweza kuleta hatari kwa abiria na mali zao.
“Pia, tuliona kivuko hicho nacho kisimamishwe ili kifanyiwe matengenezo hayo ya dharura, ikiwamo kurekebisha mbao zilizojengwa kwenye kivuko hicho, ambazo zimekuwa zikileta usumbufu na kuhatarisha maisha ya abiria,” alisema.
Ndikilo alisisitiza kuwa Tamesa chini ya Chambo ambaye alifika eneo la tukio jana, imechukua hatua za dharura kufungua injini iliyopasuka ya Mv Kilombero II na inatarajiwa kupelekwa Mang’ula ili kuchomelewa.
Pia, alisema Serikali imejipanga kuleta injini mpya inayotarajiwa kuwasili Kilombero kati ya wiki moja au mbili zijazo, ili kuziba pengo la injini iliyoharibika.
“Matengenezo tutakayoyafanya pale Mang’ula ni ya dharura tu, kuwezesha huduma zisisimame kwa muda mrefu, tuna matumaini baada ya injini hiyo kurekebishwa itarejeshwa na kufungwa kwenye kivuko ndani ya siku chache zijazo,” alisema.
Aliwaomba wananchi na wasafiri wanaotumia vivuko vya mto huo kuwa wavumilivu kwa madai kuwa, kutokea kwa hitilafu kama hiyo ni jambo la kawaida kutokana na vifaa hivyo kuwa ni vyombo vya moto. Habari hii imeandikwa na
Venance George wa Mwananchi Morogoro




Tuesday, August 23, 2011

Mbunge Silima aliyenusurika jana afariki dunia

Marehemu mbunge Silima

MBUNGE mteule kutoka Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Mussa Khamis Silima, ambaye alipata ajali juzi katika aneo la Nzuguni, Dodoma, amefariki dunia leo. Pichani juu: Marehemu akiwa katika machela baada ya kushushwa kwenye gari juzi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, akitokea Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam, alikoletwa na ndege kutoka Dodoma pamoja na gari alilopata nalo ajali. Mke wa marehemu, Mwanaheri Fahari nae alifariki katika ajali hiyo na kuzikwa jana na dereva wao Chezani Sebunga alijeruhiwa.

Mwanawe Gaddafi aapa kupambana na waasi

Mwanawe Gaddafi Saif al-Islam

Mtoto wa kiume wa Kanali Muammar Gaddafi, Saif al-Islam, ambaye awali waasi walidai kuwa wamemkamata, amejitokeza katika hoteli moja inayoshikiliwa na wafuasi wa Kanali Gaddafi.

Mwandishi wa BBC Matthew Price amezungumza na Saif al-islam na kusema kuwa anaonekana kuwa mchangamfu na shauku kuu.

Saif al-Islam amesema waasi wameingia kwenye ''mtego'' mjini Tripoli na kwamba wanajeshi wanaomuunga mkoni Kanali Gaddafi walikuwa ''wamevunja uti wa mgogo wa waasi hao''.

Waasi wanaopigana kuudhibiti mji mkuu wa LibyaTripoli , wamerudishwa nyuma na wanajeshi wanaomuunga mkono Kanali Muammar Gaddafi.

Lakini wakati mapigano yanapoendelea katika maeneo mbalimbali ya mji, msafara wa waasi kutoka mashariki mwa nchi ulirudishwa nyuma.

Bado hajulikani alipo Kanali Gaddafi

Jumapili iliyopita waasi walidai kuwa walikuwa wamemkamata Saif al-Islam, pamoja na familia yake.

Hata hivyo, bado Kanali Gaddafi hajulikani alipo. Nyumba yake inalindwa na wapiganaji wanaomtii.

Waasi hao walioingia mjini Tripoli jumamosi iliyopita walikaribishwa watu waliokuwa wakisheherekea katika bustani ya Green Square wakati walipowasili siku ya jumapili.

Waasi hao wamesema kuwa wameweka vizuizi katika sehemu mbalimbali za mji lakini wanakabiliwa na upinzani mkali katika baadhi ya maeneo.

Kamanda wa waasi amesema wanadhibiti asilimia 90 ya mji wa Tripoli.

Kiongozi wa Baraza la Mpito la kitaifa (NTC), Mustafa Abdel Jalil, amesema wakati wa ushindi halisi utakuwa pale watakapo mkamata Kanali Gaddafi.

Rais Obama apongeza watu wa Libya

Rais Barrack Obama amewapongeza watu wa Libya kwa kile alichokitaja kama ''kujitolea mhanga kusipokuwa kwa kawaida''. Obama amesema watu wa Libya wanakaribia kupata kile wanachohitaji.

Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa, Ban Ki-Moon naye amewakumbusha wanachama wa Umoja huo kuwa, wanajukumu la kuheshimu mahakama ya kimataifa ya jinai, ambayo imetoa hati za kuwakamata Kanali Gaddafi, mtoto wake wa kiume Saif al Islam na mkuu wake wa idara ya ujasusi.

Baadhi ya viongozi wa waasi wanasema afadhali wafunguliwe mashtaka nchini Libya na sio katika mahakama ya kimataifa ya ICC, mjini The Hague.

Attachments Dwight Howard wa Orlando Magic akutana na Rais Kikwete Ikulu

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete(kulia), Balozi wa Marekani nchini Tanzania Alfonso Lenhardt (kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na nyota wa mchezo wa kikapu nchini Marekani Dwight Howard(Katikati)wakati nyota huyo alipomtembelea Rais ikulu jijini Dar es Salaam jana.Nyota huyo anachezea klabu ya Orlando Magic.(picha zote na Freddy Maro)
Nyota mchezo wa kikapu nchini Marekani Dwight Howard akimwangalia Simba aliyekaushwa kitaalamu na kupamba lango la ikulu jijini Dar es Salaam huku akifurahia jambo na Rais Jakaya Mrisho Kikwete wakati nyota huyo alipokwenda ikulu kumsalimia Rais na kutoa ahadi ya kutoa msaada ili kukuza vipaji vya mchezo huo nchini.
Mchezaji maarufu wa mpira wa Kikapu duniani Dwight Howard akimkabidhi Rais Jakaya Mrisho Kikwete zawadi ya jezi wakati nyota huyo alipomtembelea Rais ikulu jijini Dar es Salaam jana. Dwight Howard ni mchezaji nyota wa timu ya kikapu ya Orlando Magic ya nchini Marekani.

Thursday, August 18, 2011

Grand Malt yazindua chupa ya mililita 330


KAMPUNI ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chake cha Grand Malt imezindua chupa mpya ya aina yake yenye ujazo wa mililita 330 katika kiwanda chake cha Dar es Salaam jana.

Kinywaji hicho, ambacho hakina kilevi kwa sasa kinauzwa kwenye kopo zenye ujazo wa mililita 330 lakini kuanzia leo kitapatikana kwenye chupa mpya itakayouzwa Sh1,000 kwa chupa na Sh 20,000 kwa kasha kwa bei ya reja reja.

“Chupa hii mpya itaziba pengo katika soko na kukifanya kinywaji hiki kupatikana kwa urahisi,” alisema Mkurugenzi wa Masoko wa TBL David Minja huku akisisitiza kuwa kinwaji hicho bado kitapatikana kwenye kopo pia.

Alisema Grand Malt ilizinduliwa Aprili mwaka jana lakini kwa sasa ni kinywaji namba moja kisichokuwa na kilevi Tanzania. “Tunawashukuru sana wateja wetu na umma kwa ujumla kwa kukikubali kinywaji hiki na kukifanya kiwe namba moja. Tunawahakikishia kuwa kitakuwepo sokoni muda wote ili kuendelea kuwaburudisha watanzania,” alisema Minja.

“Tunapozindua kinywaji hiki leo, tunapenda kuwahakikishia wateja wetu kuwa kinywaji kitakachouzwa kwenye chupa ni sawa na kile ambacho kinauzwa kwenye kopo, ambacho kina vitamini na mchanganyiko wa maziwa ya aina yake,” alisema Minja.

Meneja wa Grand Malt Consolata Adam alisema, “Grand Malt ilizinduliwa Tanzania mwaka jana na leo tunapozindua chupa hii mpya, tunawashukuru wateja wetu kwa kutuunga mkono.”

Alisema kinywaji hicho kimetokea kuwa bora kwa sababu ya ladha yake nzuri inayoifanya inyweke kirahisi kwa kuwa ina vitamini, laktosi yenye ladha nzuri, inayoitofautisha na malt zingine sokoni.

“Kinywaji hiki kinawafaa wafanyakazi wenye shughuli nyingi lakini pia kinafaa kwa matumizi ya nyumbani, wafanyakazi wa usiku, wanafunzi, vikao vya kibiashara na sherehe nyinginezo,” alisema Bi Consolata.

Alisema TBL itaendelea kukitangaza na kusambaza kinwaji hiki na kuhakikisha kinawafikia watanzania wengi zaidi popote walipo.

Wednesday, August 17, 2011

Dk Shein atembelea wizara mbalimbali


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo, katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar, akiwa katika mfululizo wa ratiba zake za kuzungumza na kila Wizara, katika kuhakikisha kila taasisi za wizara hiyo inatekeleza majukumu yake.

Rais wa Zabziar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk Ali Mohamed Shein,akizungumza na uongozi wa Wizara ya Habari,Utalii,Utamaduni na Michezo,katika mkutano uliojadili mambo ya utekelezaji wa majukumu ya wizara hiyo ambayo yataweza kukuza uchumi wetu na kuwaletea maendeleo wananchi,(kushoto) Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Iddi.

Rais wa Zabziar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk Ali Mohamed Shein,akifuatari na Uongozi wa Benki ya watu wa Zanzibar,PBZ,uliomualika Rais katika futari iliyowashirikisha baadhi ya wananchi mbali mbali katika Hoteli ya Zanzibar Beach Resort leo.

Baadhi ya Wananchi na wafanya biashara mbali mbali wakifutari kwa pamoja pia akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk Ali Mohamed Shein,pamoja na Uongozi wa Benki ya watu wa Zanzibar,PBZ,ulioyarisha futari hiyo ikiwa ni kila mwaka huwaalika watu mbali mbali katika Hoteli ya Zanzibar Beach Resort.

Rais wa Zabziar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk Ali Mohamed Shein, akitia chakula cha futari iliyoandaliwa na Uongozi wa Benki ya watu wa Zanzibar, PBZ, wakati aliposhiriki pamoja na viongozi wengine pia wakiwemo wafanya biashara mbali nbali, katika Hoteli ya Zanzibar Beach Resort leo. Picha na Ramadhan Othman Ikulu.

Monday, August 15, 2011

Watoto yatima wa Don Bosco Kimara Suka wapata boost


Wafanyakazi wa kitengo cha fedha ya benki ya Stanbic wakicheza ngoma ya mduara na watoto yatima wa Don Bosco Kimara Suka wakati wa hafla fupi ambapo wafanyikazi hao walitoa msaada wenye thamani ya wa Tsh milioni 2 wa fedha na vyakula mbali mbali.

Wafanyakazi wa Kitengo cha Fedha cha Benki ya Stanbic, wakiongozwa na Mkuu wa kitengo hicho Lydia Kukugonza (wa mwisho kulia) wakipiga picha ya pamoja na watoto yatima wa kituo cha Don Bosco kilichopo Kimara Suka jijini Dar es Salaam. Wafanyakazi hao walitoa msaada wa vyakula, vitu mbali mbali na fedha taslim vyenye thamani ya Tshs milioni 2 kwa kituo hicho.

Mkuu wa kitengo cha Fedha benki ya Stanbic, Lydia Kokugonza (mwisho kulia) akikabidhi hundi ya kwa Bw. Moses Ngenzi, Afisa ya elimu nyumba ya watoto yatima ya Don Bosco iliyo Kimara Suka. Benki ya Stanbic ilota msaada wenye thamani ya Tsh milioni 2 wa fedha na vyakula mbali mbali

Wafanyakazi wa kitengo cha fedha benki ya Stanbic, wakikabidhi msaada wa vyakula mbali mballi kwa viongozi wa nyumba ya watoto yatima ya Don Bosco Kimara Suka. Benki ya Stanbic wenye thamani ya milioni 2 wa fedha and vyakula mbali mbali. Picha kwa hisani ya Stanbic.

Sunday, August 14, 2011

Mafuta bei juu tena

Meneja wa Biashara wa Mamlaka ya udhibiti wa nishati na maji(EWURA)Mhandisi Godwin Samweli akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo,alipotangaza bei mpya ya mafuta,kulia ni Mkuu wa Idara ya Mawasaliano na Uhusiano Titus Kaguo. Picha na Michael Jamson

&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&

Kama ilivyo ada, na kulingana na Kanuni ya Kukokotoa bei za
bidhaa za mafuta ya petroli bei zimekuwa zikikokotolewa na kutangazwa na
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kila baada ya wiki mbili.
EWURA inatangaza bei elekezi/kikomo za mafuta ya petroli nchini zitakazoanza kutumika
kuanzia Jumatatu, Tarehe 15 Agosti 2011.
Bei hizi zimekokotolewa kwa kuzingatia kanuni mpya

iliyoanza kutumika mwanzoni mwa mwezi huu. Pamoja na kutambua bei elekezi/kikomo za bidhaa
mbalimbali za petroli nchi nzima, ni muhimu kuzingatia yafuatayo:

(a) Bei za jumla na rejareja kwa aina zote za mafuta zimepanda ikilinganishwa na bei zilizokokotolewa kwa ajili ya kuanza kutumika tarehe 1 Agosti 2011 ambazo zilitangazwa tarehe 3 Agosti 2011. Katika toleo hili bei zimepanda kama ifuatavyo: Petroli TZS 100.34 sawa na asilimia 5.51, Dizeli TZS 120.47, sawa na asilimia 6.30 na Mafuta ya taa TZS 100.87, sawa na asilimia 5.30. Mabadiliko haya ya bei za mafuta nchini yametokana na kupanda sana kwa bei ya mafuta katika soko la dunia na kuendelea kushuka kwa thamani ya Shilingi ya Tanzania ikilinganishwa na dola ya Marekani (sarafu ambayo hutumika katika manunuzi ya bidhaa za mafuta kwenye soko la dunia).

Kwa mfano, kwa viwango vya bei zilizotumika katika chapisho hili, bei katika soko la dunia zimepanda kwa wastani wa asilimia 5.42 na thamani ya shillingi ya Tanzania imeshuka kwa shilingi 47.12 (asilimia 2.96) kwa dola moja ya Marekani. Bei za jumla kwa kulinganisha matoleo haya mawili zimepanda kama ifuatavyo: Petroli TZS 110.34 sawa na asilimia 5.70; Dizeli TZS 120.47 sawa na asilimia 6.54; na Mafuta ya Taa TZS 100.87 sawa na asilimia 5.49.

(b) Bei za rejareja na za jumla zingepanda zaidi endapo formula ya zamani ingeendelea kutumika. Kwa kulinganisha vigezo vilivyo katika fomula ya zamani na fomula mpya, bei za mafuta zingekuwa kama ifuatavyo: SOURCE: EWURA

Pinda azindua ujenzi wa nyumba NHC


Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akikata utepe alipokuwa akizindua ujenzi wa nyumba za makazi za Medeli, mjini Dodoma juzi. Kushoto ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof Anna Tibaijuka.
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof Anna Tibaijika (kulia kwake) Naibu Waziri wa Ardhi, Goodluck Ole Medeye (aliyevaa kofia), Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Mchechu (kushoto) baada ya kutoka kutazama nyumba mpya zilizojengwa na shirika hilo katika uzinduzi wa wa ujenzi wa nyumba za makazi za Medeli, mjini Dodoma juzi. Kulia ni Spika wa Bunge Mama Anne Makinda.




VODACOM MISS TANZANIA WAELEKEA MOSHI


Warembo wa Vodacom Miss Tanzania 2011, wakipiga picha katika daraja la mto Wami, Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani jana wakati wakiwa safarini kuelekea mikoa ya Kanda ya Kaskazini kutembelea Mbuga za wanyama ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha utalii wa ndani nchini.

Thursday, August 11, 2011

Mbowe: Tutakwenda sote Ofisi za Manispaa na tutalala pale



Jioni ya leo hapa jijini Arusha ambapo Mweyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo Freeman Mbowe amesema kuwepo madarakani hadi 2015 kwa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete ni haki kikatiba, lakini akaonya kuwa umma unaweza kuamua vinginevyo iwapo Serikali itashindwa kuongoza kwa kujibu mahitaji na maslahi ya jamii.

Akihutubia mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika katika Viwanja vya NMC eneo la Unga Ltd mjini hapa alisema chama chake kinataka amani na ufumbuzi wa kudumu kuhusu tatizo la umeya Arusha ili kuruhusu shughuli za maendeleo na kiuchumi ziendelee kwa kufanyika mazungumzo ya haki na yenye nia njema kwa maslahi ya umma badala ya vyama kama ambavyo CCM kimekuwa ikifanya kuhusu mgogoro huo.

“Amani itapatikana kwa kutenda haki. Amani haiwezi kupatikana kwa kauli za viongozi au vitisho. Tumekubaliana na Waziri Mkuu siku 30 kumaliza mgogoro wa Umeya Arusha, baada hapo tutakwenda sote Ofisi za Manispaa na tutalala pale hadi kieleweke,” alisema Mbowe.

Alisema uamuzi wa kuwatimua madiwani ulikuwa mgumu na ulifikiwa usiku wa manane katika kikao kilichoanza Saa 3:00 asubuhi baada ya wahusika kukataa kusikiliza ushauri wa watu mbalimbali wakiwamo viongozi wa dini waliowataka kutekeleza maagizo ya Kamati Kuu.

Naye Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa alisema yeye na chama chake wapo tayari kufanya maandamano nchi nzima kutoka Mwanza hadi Ikulu ya Magogoni Dar es Salaam kumuomba Rais Jakaya Kikwete kuachia madaraka, iwapo ameshindwa kuhimili nguvu ya umma inayotaka mabadiliko na utatuzi wa matatizo kadhaa yanayoikabili taifa.

Tishio hilo la Dk Slaa linakuja miezi michache baada ya Rais Kikwete kuhutubia taifa mnamo mwezi na kueleza kwambaba, maandamano ya Chadema katika kona mbalimbali nchini yalikuwa na dhamira ya kutaka kuingia madarakani kwa mabavu licha ya kumalizika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka jana.

Alitishia kufanya maandamano ya nchi nzima ambayo atayaongoza kuanzia Mwanza hadi Ikulu ya Magogoni Dar es Salaam kumuomba Rais Kikwete kuachia madaraka kutokana na taifa kukabiliwa na matatizo mengi huku yeye akiwa ameshindwa kuyatatua.


Wenje

Mbunge wa Nyamagana, Ezekia Wenje na mwenzake wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa walisema wananchi wa majimbo yao wanaunga mkono uamuzi wa kuwatimua madiwani wasaliti huku Msigwa akienda mbali zaidi kwa kusema kila mapinduzi hutengeneza mashujaa na wasaliti wake.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Karatu, Lazaro Maasai alimuonya Mkurugenzi wa Manispaa ya Arusha kuwa ataongoza wananchi wa Arusha kumfungia nje iwapo ataendelea kuwatambua na kuwaruhusu madiwani waliofukuzwa uanachama.

Wasomalia hawawezi kusubiri tena


Mwandishi Maalum, New York

Balozi Augustine Mahiga, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, ameliambia Baraza Kuu la Usalama kwamba wananchi wa Somalia ambao wanakabiliwa na baa la njaa na ukame hawawezi kuendelea kusubiri tena.

Akizungumza kwa njia ya video teleconference kutokea Mogadishu jana Mahiga alisema zinahitajika dola za kimarekani Bilioni Moja ili kukabiliana na janga hilo la njaa na ukame.

Mahiga aliwataka wajumbe wa Baraza hilo, kuzichagiza serikali zao zichangie kwa haraka na kwa kiwango cha kuridhisha misaada ya kibinadamu kwa mamilioni ya wananchi wa Somalia.

Hata hivyo anasema, hadi wakati anazungumza na Baraza hilo, fedha au michango ambayo imekwisha tolewa na jumuia ya kimataifa ilikuwa haijafikia hata nusu ya mahitajio halisi.

“ Ninawaomba nyie wajumbe wa Baraza Kuu la Usalama, mzihamasishe serikali zenu zichangie kwa haraka na kuokoa maisha ya wasomali. Kwa ujumla niseme wasomali hawawezi kuendelea kusubiri zaidi” akasema Mahiga.
Balozi Mahiga anasema hali ni ya kutisha, watu wanapoteza maisha kwa idadi kubwa na hasa watoto wadogo.
Akizungumzia hali ya kisiasa na kiusalama na hasa baada ya wapiganaji wa Al Shabaab kuondoka mjini Mogadishu. Mahiga anasema kuondoka kwa kundi hilo kumetoa fursa lakini na changamoto pia.
“Kuondoka kwao kwa kweli ni mshango mkubwa kwetu sote. Na kumetoa changamoto na fursa pia. Fursa ya kwamba sasa Serikali ya Mpito ( TFG) kwa kushirikiana na Vikosi ya Kulinda Amani ( AMISOM)sasa wanashikilia asilimia 95 ya mji wa Mogadishu kwa mara ya kwanza. Changamoto ni namna ya kuendelea kuyashikilia maeneo hayo yaliyoachwa na kundi hilo”. anasisitiza Mahiga.
Anasema, kwa kuimarisha eneo lililoachwa na Al Shabaab kutasaida pia katika kulizuia kundi hilo lisireje tena katika maeneo ambako limeondoka.
Akabainisha kuwa baada ya kundi hilo kurudi nyuma na kutokomea katika maeneo tofauti na likiwa limegawanyika katika mkundi mawili, kumeongeza kasi ya usambazaji wa misaada ya kibanadamu kwa waathirika.
Na kwamba wananchi wengi waliokuwa wakiishi maeneo yaliyokuwa yakishikiliwa na kundi hilo, sasa wanakimbili mjini Mogadishu kutafuta chakula.
Akasema Ofisi ya kisiasa ambayo pia iko chini yake inaendelea kujipanga kwa kufanya tathmini na uchambuzi wa mahitaji halisi ambayo siyo tu yataviwezesha AMISOM na TFG kukalia maeneo yaliyoachwa na Al-Shabaab , bali kuchukua maeneo mengine zaidi na hivyo kupanua wigo wake.
Wakati huo huo Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Bi Susan Rice amesema serikali yake inaunga mkono kazi kubwa inayofanywa na Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu nchini Somalia, Balozi Augustine Mahiga.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mkutano wa Baraza Kuu. Susan Rice alisema serikali yake imekuwa ikifuatilia kwa karibu kazi nzuri na kubwa inayofanywa na Balozi Mahiga nchini Somalia . Pamoja na vikosi vya kulinda amani vya Afrika na kwamba inaunga mkono kila hatua ya juhudi hizo.
Akabainisha kuwa Marekani, nchi ambayo kwa sasa ndiyo inayoongoza kwa kutoka misaada katika Pembe ya Afrika.Itaendelea kuchangia kwa hali na mali ikiwamo misaada ya kibinadamu kwa wananchi wa Somalia. Pamoja na jitihada za kurejesha amani ya kudumu katika taifa hilo.

Wednesday, August 10, 2011

Mwili wa Jenerali Mayunga waagwa leo Lugalo


Rais wa Mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa, akitoa heshima za mwisho mbele ya Jeneza lenye mwili wa Marehemu Luteni Jenerali mstaafu, Silas Peter Mayunga, wakati wa shughuli ya kuaga iliyofanyika kwenye Kambi ya Jeshi Lugalo jijini Dar es Salaam leo Agost 10.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akitoa mkono wa pole kwa familia ya marehemu Luteni Jenerali, Silas Peter Mayunga, wakati wa shughuli ya kuaga iliyofanyika kwenye Kambi ya Jeshi Lugalo jijini Dar es Salaam leo Agost 10.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Kikwete, akitoa heshima za mwisho mbele ya Jeneza lenye mwili wa Marehemu Luteni Jenerali mstaafu, Silas Peter Mayunga, wakati wa shughuli ya kuaga iliyofanyika kwenye Kambi ya Jeshi Lugalo jijini Dar es Salaam leo Agost 10.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, Mkuu wa Majeshi, Davis Mwamunyange, Waziri wa Ulinzi, Hussein Mwiny, Mnadhimu Mkuu wa Jeshi, Shimbo na Jaji Mkuu Mstaafu, Agustino Ramadhan, wakiwa katika shughuli ya mazishi kuaga mwili wa marehemu Luteni Jenerali mstaafu, Silas Mayungi kwenye Viwanja vya Kambi ya Jeshi Lugalo leo Agost 10.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Kikwete, akisaini katika kitabu cha maombolezo ya kifo cha Luteni Jenerali mstaafu, Silas Peter Mayunga, aliyefariki hivi karibuni. Shughuli ya kugwa kwa mwili ya marehemu Mayunga imefanyika leo Agost 10, katika Kambi ya Jeshi Lugalo jijini Dar es Salaam. Picha zote na Muhidin Sufiani-OMR

Shida kubwa ya maji


Mkazi wa Migoli, Wilayani Iringa akitoka kuchota maji katika bwawa la Mtera. Maji hayo huuzwa ndoo sh 500 kutokana na uhaba wa maji unaokikabili kijiji cha Kigoli. Picha na Tumaini Msowoya.

Mama wa mapacha watatu aomba msaada kwa wadau

Mapacha watatu na mama yao.
Mapacha wakiwa katika picha ya pamoja.
NEEMA ya kupata watoto mapacha watatu kwa mpigo aliyoipata mkazi wa Manzese, Dar es Salaam, Amina Abubakar, imegeuka balaa na sasa mwanamke huyo anaomba msaada wa kuwasomesha.
Akizungumza ofisi za gazeti hili jana, Amina alisema sababu ya kuomba msaada huo ni kutokana na mapacha hao kufikisha umri wa kwenda shule wakati maandalizi aliyojitahidi kufanya hayajazaa matunda, huku muda unazidi kusogea.
Alisema hatua hiyo inatokana na mwanaume aliyekuwa na uhusiano naye kumkimbia tangu kuzaliwa kwa watoto hao miaka minne iliyopita.
Amina alisema alikuwa na uhusiano wa mapenzi na mwanaume ambaye alikuwa mfanyabiashara eneo la Mabibo, ambaye alikuwa anafika Dar es Salaam kutoka mkoani na kuondoka wakati yeye akiwa mamalishe.
Alisema baada ya kupata ujauzito, mwanaume huyo hakuonekana tena hadi anajifungua hajui alipo.
“Nilipokuja hapa wakati wanangu wakiwa na miezi minane nilipata msaada mkubwa baada ya Kampuni hii kunitoa kwenye gazeti nawashukuru sana, kwa hiyo nimerudi tena ili nione kama nitapata msaada wa kuwalipia ada,” alisema Amina.
Alisema hivi sasa anaendelea na biashara ya mamalishe, lakini kutokana na maisha kuwa magumu hata mahitaji muhimu ya watoto anashindwa kuyatimiza.
Kwa yeyote atakayeguswa anaomba awasiliane naye kupitia namba zifuatazo: 0718 263 968. Au Pia waweza kumpigia simu mwandishi wa habari hizi 0655 110 105

Habari hii imendikwa na Gedius Rwiza: SOURCE: MWANANCHI

Kizaazaa cha mafuta: Serikali yatoa tamko rasmi, BP, Engen, Oilcom na Camel Oil matatani


Mkurugenzi wa Mamlaka ya udhibiti wa Nishati ya maji na mafuta(EWURA) Haruna Masebo akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kuhusu maamuzi ya serikali yaliyofikia katika kutatua tatizo la mgomo wa wauuzaji wa mafuta.Picha na Fidelis Felix

EWURA imetoa Compliance Order ( amri ya kutii amri) kwa makampuni manne ambayo ni BP, Engen, Oilcom na Camel Oil, ambapo wanatakiwa watekeleze hatua zifuatazo:

1. Mara moja wanatakiwa kuanza kutoa huduma katika maghala yao ikiwa ni pamoja na kuanza kuuza mafuta katika vituo vya rejareja ikiwemo vituo vilivyo chini ya miliki zao;
2. Waache mara moja kitendo chochote kitakachosababisha upungufu wa makusudi wa mafuta ya petroli katika soko la Tanzania; na
3. katika kipindi cha masaa 24 wajieleze kwa nini wasichukuliwe hatua za kisheria dhidi yao kwa kukiuka matakwa ya Sheria ya Mafuta pamoja na Sheria ya EWURA.
Hebu cheki http://michuzi-matukio.blogspot.com/2011/08/tamko-la-waziri-wa-nishati-na-madini.html#links

Tuesday, August 09, 2011

Dk Migiro azindua ripoti ya utafiti na mpango wa kitaifa wa kushughulikia ukatili kwa watoto


Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa,Dk Asha Rose Migiro akizungumzia umuhimu wa Taifa kusimamia haki ya mtoto ya kuishi kwa amani na furaha bila kufanyiwa Ukatili wa aina yoyote katika Kilele cha uzinduzi wa ripoti ya Utafiti na Mpango wa Kitaifa wa kushughulikia “Ukatili kwa Watoto” na mpango wa Udhibiti wa Taifa.

Katikati ni Naibu Katibu Mkuu Umoja Mataifa Dr. Asha Rose Migiro, wa pili kushoto ni Waziri wa Maendeleo ya jamii, Jinsia na Watoto Sophia Simba, wa kwanza kushoto Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi Dr. Shukuru Kawambwa, wa Pili Kulia ni Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI (Elimu) Mh. Majaliwa Majaaliwa na wa Kwanza Kulia ni Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk Haji Mponda kwa pamoja wakikaribisha maandamano yaliyokuwa yakiingia katika viwanja vya Karimjee jana.

Waziri Mkuu Pinda akiteta na mtoto



Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akimsikiliza mtoto Oliver Stephene (9) akimwambia jambo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda wakati alipokuwa akitembelea mabanda kwenye Kilele cha Maonyesho ya Wakulima Nanenane wa Mwalimu J. K. Nyerere Mjini Morogoro Augost 8, 2011.(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Mkurugenzi wa Uhamiaji Rwanda azuru Tanzania


Kamishna Mkuu wa Uhamiaji Tanzania, Mgnus Ulungi (kushoto) akizungumza na Mkurugenzi wa Uhamiaji Rwanda Kalibata Anaclet (Katikati) kuhusu masuala mbali ya uhamiaji wakati mkurugenzi huyo aliptembelea Makao Makuu ya Idara ya Uhamiaji, Kurasini, Dar es Salaam jana. (Picha na Uhamiaji)

Kila la Kheri Miss Universe Tanzania 2011 Nelly Kamwelu




Unayemuona pichani ni Nelly Kamwelu, Miss Universe Tanzania 2011. Nelly ndiye atakayebeba bendera yetu akituwakilisha katika mashindano ya dunia ya Miss Universe ambayo kwa mwaka huu yatafanyikia huko Sao Paulo, Brazil ndani ya Credicard Hall kunako tarehe 12 September, 2011. Tunamtakia kila la kheri Nelly katika maandalizi yake. Picha zimepigwa na Mdau Moiz Hussein.
Hebu cheki hapa kwa taarifa zaidi http://www.hakingowi.com/2011/08/kila-la-kheri-miss-universe-tanzania.html